Endelea kujifunza

Umeshaingia
Jisajili sasa kwenye jukwaa la Taa ili uanze kujifunza, na fuatialia maendeleo yako, na kukusanya pointi, na uingie kwenye mashindano.Baada ya kujisajili, utapata cheti cha kielektroniki katika mada ambazo utajifunza.

Sehemu ya sasa:

Somo Kuchuma na kutafuta riziki

Katika somo hili, tutajifunza kuhusu maana ya kuchuma na kutafuta riziki, hukumu na maadili yanayohusiana na hayo.

  • Kujifunza kuhusu maana ya kuchuma na kutafuta riziki.
  • Kujua hukumu na maadili yanayohusiana na kuchuma.

Umuhimu wa mali

Mwanadamu anahitaji mali ili apate mahitaji yake ya kimsingi, kama vile chakula, kinywaji, nyumba, mavazi, na mengineyo. Pia anaitumia mali hiyo katika kupata manufaa na masilahi mengi ambayo kwayo huboresha hali ya maisha yake. Uislamu umeijali sana mali na ukaiwekea hukumu mbalimbali za kisheria zinazohusiana na kuichuma na kuitumia.

Maana ya kuchuma na kutafuta riziki

Ni kila njia na kazi zote ambazo mtu hufanya ili kupata mali na mambo yenye kusimamisha maisha yake, sawa iwe kupitia biashara, au kuunda bidhaa, au kilimo, au mengineyo.

Hukumu ya kuchuma na kutafuta riziki

١
Kuchuma na kutafuta riziki kunaweza kuwa ni lazima kwa mtu mwislamu binafsi katika hali fulani tofautitofauti, kama vile kuchuma kile kinachomtosha yeye na familia yake, na ili kuitumia mali hiyo kwa wale ambao anapaswa kuwapa matumizi, au kama ni kwa ajili ya kulipa madeni, au kwa ajili ya kujiweka mbali na kile kilicho mikononi mwa wengine.
٢
Kuchuma kunakuwa ni jambo linalopendekezwa ikiwa ni kwa ajili ya kutekeleza ibada za Sunna na mambo ya kumuweka mtu karibu na Mwenyezi Mungu, kama vile kuunga jamaa wa mtu kwa hilo au kumliwaza maskini.
٣
Kuchuma mapato kunaruhusiwa ikiwa ni kwa ajili ya kufurahia na kustareheka na kile ambacho Mwenyezi Mungu ameruhusu katika vyakula, vinywaji, mavazi, na vitu vingine vilivyoruhusiwa zaidi ya mahitaji ya kimsingi.
٤
Kuchuma mapato ni haramu ikiwa yalipatikana kwa njia iliyoharamishwa, au ikiwa humsababisha mtu kuacha mambo ya faradhi au kuingia katika mambo yaliyoharamishwa.
٥
Kuchuma kunaweza kuwa jambo la kuchukiza ikiwa kuko nje ya yale yaliyotangulia, kama vile ikiwa kunamshughulisha akaacha ibada za sunna.

Ikiwa nia ya kuchuma mapato ni kujivuna na kukithirisha mali, basi hilo linakuwa jambo la kuchukiza. Na kwa mujibu wa baadhi ya wanasheria linakuwa haramu.

Mwislamu anayejitahidi kuchuma na kutafuta mapato ni lazima apate maarifa yanayohusiana na hili, kwa kuzijua hukumu za miamala inayohusiana na mali, kama vile hukumu za uuzaji, mkataba wa kukodisha, kampuni, riba, na miamala mingine anayofanya, ili asiingie katika jitihada zake hizo za kutafuta riziki katika kile ambacho Mwenyezi Mungu aliharamisha.

Adabu za kuchuma na kutafuta riziki

1- Mojawapo ya maadili ya lazima katika kutafuta riziki ni kutochelewesha au kuzuia maagizo yoyote miongoni mwa maagizo ya Mwenyezi Mungu. Maagizo haya yanapaswa kuwa msingi unaodhibiti wakati na juhudi za Mwislamu kwa kuifuata misingi hiyo.

2. Katika adabu za wajibu pia ni kwamba kutafuta riziki kwa Muislamu kusisababishe kuwadhuru wengine, kwa maana haifai kumdhuru mtu wala kujidhuru mwenyewe.

3- Kwamba mtu akusudie makusudio mazuri katika kutafuta riziki, kama vile kujizuia kuwaomba watu, na kutumia mali zake kuwapa matumizi wale ambao analazimika kuwasimamia, na pia kutumia mali hiyo katika kufanya mambo ya utiifu. Kwa hivyo nia yake isiwe ni kukusanya mali, kuizidisha, na kujivuna kwayo au nia nyinginezo potovu.

Ikiwa Mwislamu ni mkweli katika kutafuta riziki, na anakusudia kwa hilo kupata kile anachoweza kuwapa watu sadaka, basi anakuwa kwenye ibada katika kutafuta kwake huko, na kwa hilo anafikia hadhi ya juu. Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimfikie, "Watu wanaopendwa zaidi na Mwenyezi Mungu ni wenye kuwaufaisha zaidi watu." (Al-Awsat cha Tabarani 6026)

4. Kufanya wastani na uwiano kati ya kutafuta riziki na mahitaji mengineyo ya kibinadamu, ili kwa hivyo isiwe kwamba kuchuma ambako ni njia tu kunabadilika na kuwa ndilo lengo. Salman alimwambia Abu Dardaa, Mwenyezi Mungu awaridhie: "Hakika, Mola wako Mlezi ana haki juu yako, na nafsi yako ina haki juu yako, na familia yako ina haki juu yako. Kwa hivyo mpe kila mwenye haki, haki yake." Basi Abu Dardaa akamjia Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimfikie na akamtajia hayo. Mtume (rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimfikie) akasema: "Salman amesema ukweli."(Al-Bukhari 1968)

5- Kumtegemea Mwenyezi Mungu katika kutafuta riziki. Uhakika wa kumtegemea ni kwamba mwanadamu afanye visababu halali, na aufungamanishe moyo wake na Mwenyezi Mungu.

6- Mtu awe na yakini kwamba riziki haitoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu peke yake, na kwamba haitokani na kuchuma kwenyewe. Kwa maana, anaweza kufanya visababu vya kufikia riziki, lakini asiipate, kwa sababu ya hekima fulani anayoijua Mwenyezi Mungu.

7- Kuridhika na kile ambacho Mwenyezi Mungu amempa na asione kwamba riziki inamjia polepole. Riziki imekadiriwa kabla na Mwenyezi Mungu kwa wakati na kiasi chake. Kwa hivyo Muislamu anafaa kutafuta riziki kwa adabu, kuridhika, na kutosheka na yale ambayo Mwenyezi Mungu amemuandikia, akitafuta halali na akijiweka mbali na haramu. Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alisema: "Enyi watu! Mcheni Mwenyezi Mungu na muwe wazuri katika kutafuta. Kwani hakuna nafsi itakufa mpaka ipate riziki yake kamili, hata kama ni itachukua muda kuijia. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na muwe wazuri katika kutafuta. Chukueni kilicho halali, na acheni kilichoharamishwa." (Ibn Majah 2144)

Umemaliza somo kwa ufanisi


Anza mtihani