Endelea kujifunza

Umeshaingia
Jisajili sasa kwenye jukwaa la Taa ili uanze kujifunza, na fuatialia maendeleo yako, na kukusanya pointi, na uingie kwenye mashindano.Baada ya kujisajili, utapata cheti cha kielektroniki katika mada ambazo utajifunza.

Sehemu ya sasa:

Somo Maana na fadhila zake

Swala ina hadhi kubwa katika Uislamu, nayo ni moja ya nguzo zake kubwa, na nguzo muhimu katika maisha ya Muislamu. Katika somo hili, utajifunza kuhusu maana ya Swala, hadhi yake na fadhila zake.

  • Kujifunza maana ya Swala.
  • Kujifunza hadhi ya Swala katika Uislamu.
  • Kujifunza fadhila za Swala na umuhimu wake.

Maana ya Swala

Maana ya swala katika lugha ni dua. Swala ni mafungamano kati ya mja na Mola wake Mlezi, Muumba wake, kwani inajumuisha maana za juu kabisa za uja na kutafuta kimbilio kwa Mwenyezi Mungu na kuomba msaada wake. Ndani yake mja anamuomba, na kumnong'oneza na kumkumbusha, basi nafsi yake inakuwa safi, na anakumbuka uhakika wake na uhakika wa dunia hii anayoishi, na anahisi ukubwa wa Mola wake Mlezi na rehema yake kwake. Kisha hili linamuongoza kushikamana na sheria ya Mwenyezi Mungu na kujiepusha na dhuluma, uchafu, na uasi. Kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Swala inazuilia mambo machafu na maovu." (Al-Ankabut: 45)

Hadhi ya Swala

Swala ndiyo ibada kubwa zaidi ya kimwili na yenye hadhi kubwa zaidi ya ibada zote. Ni ibada inayojumuisha moyo, akili, na ulimi. Umuhimu wa swala unaonekana katika mambo mengi, ikiwa ni pamoja na:

1. Ni nguzo ya pili ya Uislamu. Kwani amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Uislamu umejengwa juu ya mambo matano: kushuhudia kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu na kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na kusimamisha Swala...” (Al-Bukhari 8, Muslim 16) Hii ni kwa sababu nguzo ya jengo ni msingi wake ambao jengo hilo linautegemea na wala hauwezi kusimama bila huo.

2. Ndiyo huleta tofauti baina ya Waislamu na makafiri, kwani Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, amesema: “Baina ya mtu na ushirikina na ukafiri ni kuacha Swala.” (Muslim 82) Na akasema: “Ahadi iliyo baina yetu na wao ni Swala. Kwa hivyo, mwenye kuiacha, basi hakika amekufuru.” (Tirmidhi 2621, Nasai 463)

3. Mwenyezi Mungu Mtukufu aliamuru kwamba ihifadhiwe katika hali zote, wakati wa safari, nyumbani, katika hali ya amani, katika vita, na katika afya na maradhi, na ifanywe kwa kiasi inavyowezekana, kama Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyosema: "Zilindeni Swala." (Al-Baqara: 238) Na aliwaelezea waja wake waumini kwa kauli yake: "Na ambao Sala zao wanazihifadhi." (Al-Mu’minun: 9)

Fadhila za Swala

Kuna ushahidi mwingi kuhusiana na fadhila za swala kutoka katika Qur-ani na Sunna, ikiwa ni pamoja na:

1. Inafuta madhambi. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Swala tano za kila siku, Ijumaa hadi Ijumaa, na Ramadhani hadi Ramadhani, zinafuta yale yaliyo baina yake ikiwa mtu atajiepusha na madhambi makubwa.” (Muslim 233), Tirmidhi 214)

2. Ni nuru ing’aayo kwa Muislamu katika maisha yake yote, ikimwita kwenye heri na kumuepusha na maovu. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Hakika Swala inakataza machafu na maovu." (Al-Ankabut: 45) Na amesema Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Swala ni nuru.” (Muslim 223)

3. Ndilo jambo la kwanza ambalo mja ataulizwa Siku ya Kiyama. Ikiwa swala yake itakuwa nzuri na ikakubaliwa, basi matendo yake mengine yote yatakubaliwa. Na ikiwa itakataliwa, basi matendo yake mengine yote yatakataliwa. Kama alivyosema Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Jambo la kwanza ambalo mja atahesabiwa kwalo Siku ya Kiyama ni swala. Ikiwa swala yake itakuwa nzuri, basi matendo yake yote yatakuwa mazuri.” (Al-Mu’jam Al-Awsat cha Tabarani 1859)

Swala ndio wakati mtamu zaidi kwa muumini wakati anapokuwa ananong'ona humo na Mola wake Mlezi, kwa hivyo, anapata raha, utulivu, na kuhisi uwepo wa urafiki kati yake na Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Na ilikuwa swala ndiyo ladha kubwa zaidi kwa Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kama alivyosema: “Na imewekwa furaha ya jicho langu katika swala.” (Nasai 3940)

Swala ndiyo raha ya Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake

Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alikuwa akimwambia muadhini wake, Bilal, anapoadhini kwa ajili ya swala, "Ewe Bilal, simamisha Swala na utupe raha kwayo.” (Abu Dawud 4985)

Kila mara Nabii, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipokuwa anapatwa na wasiwasi kubwa, anakimbilia kuswali. (Abu Dawud 1319)

Umemaliza somo kwa ufanisi


Anza mtihani