Endelea kujifunza

Umeshaingia
Jisajili sasa kwenye jukwaa la Taa ili uanze kujifunza, na fuatialia maendeleo yako, na kukusanya pointi, na uingie kwenye mashindano.Baada ya kujisajili, utapata cheti cha kielektroniki katika mada ambazo utajifunza.

Sehemu ya sasa:

Somo Masharti na hukumu za swala

Swala ina masharti ambayo haiwi sahihi bila ya hayo, kwa hivyo inamlazimu Muislamu ayafahamu masharti haya. Katika somo hili, utajifunza kuhusu masharti ya swala, hukumu yake na nafasi yake.

  • Kujua masharti ya swala.
  • Kujua  hukumu ya swala.
  • Kujua kuhusu hukumu za mahali pa kuswalia.

Masharti ya swala

1. Twahara

Twahara kutokana na hadathi na najisi. Imesimuliwa kutoka kwa Abdullah bin Umar, Mwenyezi Mungu awe radhi nao wote wawili, kuwa alisema: Nimemsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akisema: “Haikubaliki swala bila ya twahara.” (Muslim 224)

2. Kufunika sehemu za siri za mtu

Ni sharti kusitiri uchi kwa nguo ambayo haionyeshi viungo kwa sababu ya ufupi au uwazi wake.

Uchi wa mwanamume

Kuanzia katika kitovu hadi katika magoti

Uchi wa mwanamke katika swala

Ni mwili wake wote isipokuwa uso na mikono. Imesimuliwa kutoka kwa Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: Amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Mwenyezi Mungu haikubali Swala ya mwenye hedhi [yaani, mwanamke mtu mzima] isipokuwa awe amejifunika kwa kitambaa.” (Abu Dawuud 641, na Tirmidhi 377)

Na Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema, "Enyi wanaadamu! Chukueni pambo lenu kwenye kila pahala wakati wa ibada." (Al-A'raf: 31) Na kufunika tupu ndiko pambo la chini zaidi.

3. Kuelekea Kibla

Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema, "Na popote wendako, elekeza uso wako kwenye Msikiti Mtakatifu." (Al-Baqara: 149)

Ni kipi kibla cha Waislamu?

Kibla cha Waislamu ni Al-Kaaba tukufu iliyojengwa na baba wa Mitume, Ibrahimu amani iwe juu yake, na wakahiji huko Mitume wote, amani iwe juu yao. Tunajua kwamba ni mawe tu ambayo hayadhuru wala hayanufaishi, lakini Mwenyezi Mungu Mtukufu alituamuru tuielekee huko katika swala ili Waislamu wote waungane katika mwelekeo mmoja, na kwa kuelekea huko tukawa tumemwabudu Mwenyezi Mungu.

Jinsi ya kuelekea kibla

Cha wajibu kwa Muislamu ni kuelekea Al-Kaaba akiiona mbele yake. Ama aliye mbali, inamtosheleza kuelekeo upande wa Makka, na kugeuka mbali nayo kidogo hakudhuru kitu. Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: “Kati ya mashariki na magharibi ni Kibla.” (Tirmidhi: 342)

Je, mtu ambaye hawezi kuelekea Kibla kwa sababu ya maradhi au mengine afanye nini?

Wajibu huo unaondolewa kwake kwa sababu ya kutokuwa na uwezo, kama vile faradhi zote huondolewa kwa sababu ya kutoweza kuzitekeleza. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Basi mcheni Mwenyezi Mungu kama mwezavyo." (At-Taghabun: 16)

4. Kuingia wakati wa swala

Ni sharti ili swala iwe sahihi, na wala swala haiwi sahihi kabla ya muda wake kuingia, na imeharamishwa kuichelewesha zaidi ya wakati wake. Kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Kwani hakika Swala kwa Waumini ni faradhi iliyowekewa nyakati maalumu." (An-Nisa: 103)

Ni bora zaidi kutekeleza swala mwanzoni mwa wakati wake. Imesimuliwa kutoka kwa Ummu Farwa, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: Aliulizwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: Ni matendo gani yaliyo bora zaidi? Akasema: “Ni swala mwanzoni mwa wakati wake.” (Abu Dawud 426)

Je, inaruhusika kuchelewesha swala zaidi ya muda wake uliowekwa?

Swala ni lazima iswaliwe kwa wakati wake, na ni haramu kuichelewesha isipokuwa katika hali ambayo inaruhusika kuunganisha Swala mbili.

Je, mtu anayekosa swala kwa sababu ya usingizi au kusahau afanye nini?

Ni lazima aharakishe kuilipa mara atakapokumbuka. Imesimuliwa kutoka kwa Anas bin Malik, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu: “Mwenye kusahau Swala au akalala ikampita, basi kafara yake ni kuiswali wakati anapoikumbuka.” (Muslim 684)

Ulazima wa swala

Swala ni wajibu kwa kila Mwislamu mwenye akili timamu, asiyekuwa na hedhi na nifasi. Yeye hapaswi kuswali muda wa hedhi yake au nifasi yake, na wala halazimiki kuzilipa swala hizo baada ya kusafika kwake na damu yake kwisha.

Mtu anahukumiwa kuwa amebaleghe ikiwa moja ya ishara zifuatazo zitapatikana:

١
Kufikia umri wa miaka kumi na tano
٢
Kuota nywele ngumu kwenye uchi wa mbele
٣
Kutokwa manii katika ndoto au hali ya kuwa yuko macho
٤
Mwanamke kupata hedhi au kupata mimba

Swala tano za wajibu na nyakati zake

Mwenyezi Mungu amemuwajibishia Muislamu swala tano usiku na mchana. Hizo ndizo nguzo za dini yake, na wajibu uliosisitizwa zaidi juu yake, nazo zimeekewa nyakati dhahiri kama ifuatavyo:

Swala ya al-fajr

Ni rakaa mbili, na wakati wake huanza kwa kuchomoza alfajiri ya pili, ambayo ni mwanzo wa mwanga kwenye upeo wa macho kutokea upande wa mashariki, na inakwisha kwa kuchomoza jua.

Swala ya Dhuhr

Ni rakaa nne, na wakati wake huanza pindi jua linapoanza kuelekea upande wa magharibi baada ya kupita katikati ya mbingu, na huisha pale kivuli cha kila kitu kinapokuwa sawa na urefu wake.

Swala ya Asr

Ni rakaa nne, na wakati wake unaanzia wakati swala ya adhuhuri inapoisha, ambapo kivuli cha kila kitu kinakuwa sawa nacho, na inamalizika kwa kuzama jua. Na Muislamu anapaswa kuharakisha kuswali kabla ya miale ya jua kudhoofika na kuwa ya njano.

Swala ya Maghrib

Ni rakaa tatu, na wakati wake huanza kwa kuzama jua na kutoweka kwake kwenye upeo wa macho, na huishia na kuzama kwa utusiutusi mwekundu ambao huonekana baada ya jua kuzama.

Swala ya Ishaa

Ni rakaa nne, na wakati wake huanza kwa kutokea utusiutusi mwekundu na humalizika usiku wa manane, na inaweza kuiswali wakati wake wa mwisho zaidi karibia alfajiri.

Hadhi ya swala

Uislamu uliwaamuru wanaume kuswali katika jamaa (mkusanyiko), na ulitaka hili liwe msikitini, ili kuwepo kongamano na mkusanyiko wa Waislamu, ili yaongezeke mafungamano ya udugu na mapenzi baina yao, na akalifanya hilo kuwa bora kwa daraja nyingi kuliko mtu anayeswali peke yake. Kama alivyosema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: “Swala ya jamaa ni bora kuliko swala ya mtu binafsi kwa daraja ishirini na saba.” (Al-Bukhari 645, Muslim 650, Ahmad 5921)

Masharti yanayohusiana na mahali pa kuswalia

Uislamu umeweka sharti kwamba mahali pa kuswalia pawe kwenye ardhi iliyo safi, Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema: “Na tuliagana na Ibrahim na Ismail: Itakaseni Nyumba yangu kwa ajili ya wanaoizunguka kwa kutufu na wanaojitenga huko kwa ibada, na wanaoinama na kusujudu.” (Al-Baqara: 125)

Hali ya asili ni usafi wa mahali pa kuswalia

Na hali ya asili ni kwamba mahali hapo ni safi, na najisi ni kitu kilichopaingilia tu. Kwa hivyo maadamu hujui uwepo wa najisi mahali hapo, basi pahukumu kwamba ni mahali safi. Na inaruhusika kuswalia juu ya mahali popote palipo safi, wala mtu halazimiki kutafuta mkeka au shuka ambayo mtu hawezi kuswali isipokuwa juu yake tu.

Kuna masharti ya jumla ya mahali pa kuswalia ambayo mwenye kuswali anapaswa azingatie, miongoni mwake ni:

1. Kwamba asiwaudhi watu katika mahali pake pa kuswalia, kama vile mtu anayeswalia katika njia zilizopitiwa na mahali wanapopita watu, na mahali popote panapokatazwa kusimama hapo, ili kutosababisha msongamano na kusumbua watu. Na Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, amekataza kuudhi na kudhuru, akisema: “Hakuna kudhuru wengine wala kujidhuru.” (Ibn Majah 2341, Ahmad 2865)

2. Pasiwe na kitu cha kumshughulisha mwenye kuswali, kama vile picha, sauti kubwa, au muziki.

3. Kwamba mahali hapo pasiwe pameandaliwa hasa kwa ajili ya kumuasi mwenyezi Mungu, kama vile disko na vilabu vya usiku, kwani inachukiza kuswalia hapo.

Umemaliza somo kwa ufanisi


Anza mtihani